Nyumba

Nyumba ni jengo lenye shabaha ya kuwapa watu makazi na nafasi ya kuishi humo. Watu walianza kujenga nyumba tangu miaka mielfu mingi kama kinga dhidi ya hali ya hewa na athari za jua, usimbishaji au baridi. Nyumba ni makazi ya kudumu tofauti na makazi ya muda kama hema.

Nyumba ya Kasbah nchini Moroko hujengwa kwa udongo ulioshindiliwa

Kuna nyumba ndogo yenye chumba kimoja tu lakini kuna pia nyumba zenye vyumba mamia. Pale ambako nafasi ya kujenga ni haba kuna nyumba za ghorofa. Kiasili maghorofa yalijengwa pia kwa sababu za usalama.

Sehemu za nyumba

Nyumba huwa na ukuta na paa. Kila nyumba inahitaji mlango; kama nyumba ni ndogo mlango huu unaweza kutosheleza pia mahitaji ya mwanga. Nyumba nyingi huwa pia na madirisha kwa kuingiza nuruna hewa.

Aina za nyumba

Nyumba ya kijijini nchini Rwanda; udongo na ubao
Nyumba ya karne ya 15 inayong'ing'inia mjini Cuenca, Hispania

Katika nchi za joto nyumba za utamaduni asilia mara nyingi hujengwa nyepesi. Penye joto hakuna sababu ya kuwa na kuta nene za kuzuia baridi. Paa inahitaji kuwapa wenyeji kivuli wakati wa mchana na kinga dhidi ya mvua wakati wa masika.

Vifaa vya ujenzi

Nyumba hutofautiana na mazingira na hali ya hewa, halafu kutokana na vifaa vya ujenzi kama udongo, ubao, matofali, simiti na kadhalika.

Katika utamaduni asilia vifaaa hivi vilichaguliwa na hadi leo huchaguliwa kutokana na vile vinavyopatikana katika mazingira. Penye misitu mingi ujenzi kwa kutumia ubao ni kawaida.

Penye milima na miamba kuna ujenzi kwa mawe yaliyochongwa. Nyumba hizi huwa ni imara sana. Lakini pasipo na miamba ni ghali sana kusafirisha mawe yale kutoka mbali kwa hiyo watu wametumia udongo au ubao au zote mbili kwa pamoja.

Pasipo na mvua nyingi na penye udongo wa kufaa ni rahisi kujenga ukuta kwa kutumia mafimbo yanayopakwa kwa udongo. Katika Afrika ya Kaskazini Waberberi wanajua namna ya kuchanganya aina mbalimbali za udongo na kuuponda kati ya bao za kando. Kwa njia hii wamejenga nyumba za ghorofa nyingi kwa mfano kasbah wakatumia ubao kwa sakafu za ghorofa tu.

Waswahili wa miji ya pwani la Afrika ya Mashariki walitumia vipande vya jiwe la matumbawe liliochangaywa na udongo. Nao hao walijenga nyumba za ghorofa kwa njia hiyo. Upana wa vyumba ulitegemea urefu wa miti ya mikoko iliyopatikana kwa sababu walitumia pia ubao hasa kwa sakafu za kila ghorofa.

Katika nchi nyingi watu wamegundua mbinu wa kujenga nyumba kwa kutumia matofali. Penye hali ya hewa kavu hutumia matofali yaliyokauka tu; lakini penye udongo wa ufinyanzi na ubao wa kutosha waliendelea kuchoma matofali yanayokuwa magumu kama mwamba laini.

Teknolojia ya saruji imebadilisha ujenzi wa nyumba mahali pengi hasa pamoja na upatikanaji wa vyuma kila mahali. Sarufi inaruhusu kujenga kwa nyumba imara kama mwamba lakini haihitaji kazi ya kukata. Penye mawe kwa bei nafuu bado mawe huendelea kutumiwa hasa kwa sababu zinapendeza kwa kuta za nje ila tu hata hapa mara nyingi mihimili ya saruji na chuma zinaingizwa kama kiunzi na kuboresha uimara.

Vipande vya nyumba ya kiwandani vinaunganishwa
Kipande cha nyumba ya kiwandani kinashikwa na winchi

Nyumba zilizoandaliwa kiwandani

Katika nchi zilizoendelea nyumba hutengenezwa kiwandani kisehemu. Mahali pa nyumba huandaliwa kwa kumwaga saruji ya sakafu na kuweka tayari mabomba ya maji na maji machafu pamoja na umeme na simu mahali panapotakiwa kulingana na mipango.

Baada ya kukauka kwa msingi huu sehemu nyingine zinaweza kuungaishwa juu yake. Kuta za nje na ndani pamoja na milango, madirisha, mabomba na nyaya zinatengenezwa tayari katika kiwanda na kupelekwa mahali pa ujenzi kwa lori. Wafanyakazi wachache wanaunganisha vipande kuwa nyumba kamili kwa msaada wa winchi .

Kuta za ndani hutengenezwa mara nyingi kwa aina za bao zinazotengenezwa kwa kutumia nyuzi pamoja na sarufi au jasi tu. Bao za aina hii ni nyepesi na rahisi.

Nyumba maskini katika mtaa wa vibanda mjini Jakarta (Indonesia)

Jumba

Jumba ni jina la nyumba kubwa sana kwa mtu au familia moja. Nyumba za wafalme zaitwa mara nyingi "jumba". Kuna pia matajiri wanaojenga majumba.

Majengo ya ina tafautiana. Kinshasa, Luanda, Nairobi

Mufano: Mbarara;[1]

Kati ya majumba yanayojulikana sana duniani ni Jumba la Kifalme la Versailles au majumba ya Mji Haramu wa Beijing. Jumba linalotajwa mara nyingi kwenye habari ni Jumba la Kifalme la Buckingham Palace mjini London kwa sababu wafalme na malkia wamepokea wageni rasmi huko tangu miaka mingi.

Viungo vya nje

WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mambo ya utamaduni bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Nyumba kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.