Antena

Antena au erio (Kiing. antenna - aerial) ni kifaa cha kurusha au kupokea mawimbiredio ikiwa ni kiungo au kikusa (interface) kati ya mawimbiredio yanayopita kwenye waya ya umeme na mawimbiredio yanayosambaa hewani.

Antena mbalimbali.

Mara nyingi antena hutumiwa pamoja na transmita (kifaa cha kurushia mawimbi ya redio) au risiva (kifaa cha kupokelea mawimbiredio). Katika urushaji wa mawimbi, transmita ya redio huipa antena nguvu ya kiumeme (mkondo wa umeme) katika ncha zake na hivyo antena hutoa mawimbi ya radio kutegemeana na mkondo wa umeme yenye tabia za ki-umeme na ki-sumaku (electromagnetic radiation, electromagnetic waves).

Kwa upande wa risiva, antena hupokea mawimbi ya redio yaliyotumwa na transmita na kuyabadilisha kuwa mkondo wa umeme kwenye ncha zake na kupelekwa kwenye amplifaya.

Antena ni vifaa muhimu sana kwa vifaa vyote vitumiavyo mawimbi ya redio. Hutumika katika mifumo mbalimbali kama vile mitambo ya kurushia matangazo ya redio, matangazo ya televisheni, risiva za mawasiliano, rada, simu ya mkononi, satelaiti na vitu vingine kama vile vifaa vya kufungulia milango ya karakana (gereji), mitandao ya kompyuta isiyotumia nyaya na kadhalika.[1][2][3]

Marejeo