Dini nchini Urusi

Dini nchini Urusi zimepata uhai mpya na kustawi tena tangu Ukomunisti uanguke mwaka 1989.

Mchoro wa Ivan Eggink ukionyesha Vladimir Mkuu akisikiliza mapadri wa Kiorthodoksi, huku mjumbe wa Papa akinuna pembeni.
Ubatizo wa Vladimir, mchoro wa ukutani wa Viktor Vasnetsov

Wafuasi wa dini hawahesabiwi katika sensa, hivyo kuna makadirio tu. Kwa jumla Waslavi mara nyingi ni Wakristo wa Kiorthodoksi, wasemaji wa lugha za Kiturki ni zaidi Waislamu, na wenye lugha za Kimongolia mara nyingi hufuata Ubuddha.[1]

Mnamo Agosti 2012 kulikuwa na kadirio la asilimia 46.8 za Warusi kuwa Wakristo [2] na asilimia 25 waliamini uwepo wa Mungu lakini bila kufuata dini yoyote. Makadirio mengine yalitaja asilimia 76 za Warusi kuwa Wakristo au asilimia 65.

Ukristo

Warusi wengi kabisa walikuwa wafuasi wa Ukristo wa Kiorthodoksi hadi mapinduzi ya Urusi ya 1917/18.

Katika mapokeo yao wenyewe ni Mtume Andrea aliyeleta mara ya kwanza imani hiyo hadi Urusi.[3].

Kihistoria ni kwamba mwaka 988 mtemi wa Kiev Vladimir Mkuu alipokea ubatizo kutoka kwa mapadre wa Kanisa la Bizanti uliofuatwa na ubatizo wa familia na wananchi wa Kiev[4]). Tukio hilo liliathiri moja kwa moja utamaduni wa Urusi, Ukraina na Belarus pamoja na historia yote iliyofuata.

Kanisa la Kiorthodoksi liliendelea kuwa dini rasmi katika milki za Kirusi hadi mapinduzi ya 1917.

Wakomunisti walioshika utawala mwaka ule walikataa dini zote [5] Urusi pamoja na Umoja wa Kisovyeti ilikuwa nchi ya kwanza iliyoamua kufuata uatheisti kama itikadi kuu[6] [7][8]

Dini za awali ziliendelea chini ya ukomunisti lakini kwa matatizo makubwa. Waumini waliweza kusali kwao nyumbani na katika makanisa na misikiti michache iliyobaki. Wakati wa Vita Kuu ya Pili mateso yalipungua kidogo kwa sababu Joseph Stalin alitaka kuwaunganisha wananchi wote chini ya uongozi wake katika juhudi za vita.

Serikali ya kikomunisti ilinyang'anya mali na majengo ya Kanisa, magazeti yake yalishambulia mafundisho ya dini, uatheisti ukafundishwa shuleni na waumini wakahangaishwa.[9] Makanisa mengi yaligeuzwa kuwa ghala, ukumbi wa michezo na kadhalika au kubomolewa.

Mapadre, maaskofu na wamonaki mara nyingi walikamatwa, kutupwa gerezani au kutumwa kwenye makambi ya GULAG. Kati ya miaka 1922 hadi 1926 jumla ya maaskofu 28 na mapadre zaidi ya 1,200 waliuawa. Wengi sana zaidi walidhulumiwa.[10]

Upande wa Wakristo, wengi wanakadiriwa kuwa Waorthodoksi (kati ya hao wengi hawashiriki kwenye ibada za mara kwa mara) na wachache ni Wakatoliki na Waprotestanti.

Hekalu la dini zote mjini Kazan, Tatarstan

Uislamu

Uislamu ni dini yenye wafuasi wengi baada ya Kanisa la Kiorthodoksi.[11] Ni dini kuu kati ya watu wengi wa Kaukazi kama vile Wachecheni, Waingushi na Wacherkesi, pia kati ya wasemaji wengi wa Lugha za Kiturki kama vile Watatari na Wabashkiris. Kwa jumla kuna kadirio la kuwepo kwa milioni 9,400,000 Waislamu ambao ni sawa na asilimia 6.5% ya wananchi wote. Walio wengi ni Wasunni, pamoja na wafuasi wachache wa Shia na Ahmadiya. Sehemu kubwa wanajihesabu kuwa Waislamu bila madhehebu.[12] [2][13]

Dini nyingine

Katika maeneo matatu kuna wafuasi wa Ubuddha ambayo ni Buryatia, Tuva na Kalmykia.

Dini za jadi hufuatwa bado katika sehemu za Siberia na Mashariki ya Mbali kama vile Yakutia na Chukotka.

Wasio na dini

Kuhusu watu wasio na dini kuna makadirio kuwa kati ya 16% na 48% ya wananchi wote.[14]

Idadi ya watu wanaojihesabu kuwa Waatheisti ni asilimia 7 na idadi yao imeendelea kupungua.

Tanbihi

Makala hii kuhusu mambo ya dini bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hii kama historia yake au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.