Guinea Mpya ya Kiholanzi

Guinea Mpya ya Kiholanzi ilikuwa koloni la Uholanzi kwenye sehemu ya magharibi ya kisiwa cha Guinea Mpya kutoka mwaka 1949 hadi 1962. Leo hii ni sehemu ya Indonesia ikiwa ni majimbo ya Papua na Papua Magharibi.

Ramani ya Guinea Mpya ya Kiholanzi
Bendera ya Guines Mpya ya Kiholanzi

Ilikaliwa tangu milenia kadhaa na Wapapua ambao ni jina la kutaja jumla la wenyeji ikitawaliwa kama sehemu ya koloni la Uhindi wa Kiholanzi (leo Indonesia) tangu 1828; Waholanzi walianza kueneza utawala wao kisiwani katika karne ya 20 tu.

Baada ya vita ya uhuru wa Indonesia Waholanzi walikubali kuondoka Indonesia lakini walipatana kuangalia suala la Guinea Mpya baadaye. Katika mwaka uliofuata, Uholanzi lilipeleka suala hilo mbele ya Umoja wa Mataifa ikaeleza kwamba wenyeji Wapapua ni tofauti kabisa na watu wa Indonesia, hivyo wanastahili kujitawala tena pamoja na Wapapua wenzao katika sehemu ya mashariki ya kisiwa.

Katika miaka ya 1950 Uholanzi ilichukua hatua ya kuandaa koloni kwa uhuru; walimu 5,000 walitumwa kutoka Uholanzi kuboresha elimu na vikosi vya kwanza vya jeshi la kieneo vilanzishwa.

Mwaka 1957 Indonesia ilishindwa kupewa kibali cha Umoja wa Mataifa kuwa kisiwa kiwe chini yake. Waholanzi waliendelea kuandaa uchaguzi na bunge la kwanza lilitokea mwaka 1961.

Katika Indonesia rais Suharto aliwahutubia wananchi kujiandaa kwa mapambano makali ya kutwaa Guinea Mpya.[1] Kwenye Januari 1962 Indonesia ilivamia koloni. Waholanzi hawakuwa tayari kupiga vita tena, na Marekani iliwashawishi kuacha eneo hilo kwa Indonesia.

Katika mapatano ya 15 Agosti 1962 yaliyotiwa sahihi kwenye makao makuu ya UM mjini New York, eneo liliwekwa kwa muda chini ya mamlaka ya Umoja wa Mataifa kuanzia Oktoba 1961, na kwenye Mei 1961 ilikabidhiwa kwa Indonesia. Katika mapatano Indonesia ilikubali kuwapa watu wa eneo nafasi ya kupiga kura juu ya uhuru au kubaki katika Indonesia hadi mwaka 1969.[2]

Mwaka 1969, Indonesia haikutekeleza masharti, badala ya kura ya watu wote jeshi lake liliteua watu 1,025 ambao walipiga kura ya wazi; wote walikubali kubaki Indonesia. Watazamaji walisikia kutoka kwa wajumbe kwamba walitishiwa kabla ya kura wakaogopa usalama wao wenyewe na usalama wa familia zao.

Katika miaka iliyofuata, kulikuwa na upinzani dhidi ya utawala wa Indonesia iliyogandamizwa mara kwa mara na jeshi la Indonesia.[3] Kampeni ya Free West Papua Campaign inajaribu kutafuta msaada wa kitaifa kwa jitihada za uhuru[4].

Marejeo

Viungo vya Nje

Wikimedia Commons ina media kuhusu: