Kiuadudu

Kiuadudu (pia kiuawadudu, kiuatilifu au dawa ya wadudu, kwa Kiingereza: insecticide')' ni sumu au patojeni zilizoandaliwa kuua wadudu, kuwafukuza au kuchelewesha ukuaji wao.[1] Kinaweza kulenga wadudu wenyewe, mayai au lava.

Mkulima akinyunyiza kiuadudu kwenye mkorosho nchini Tanzania.

Viuadudu hutumiwa katika kilimo, tiba, tasnia na kwenye nyumba za watu. Watu hulenga kuua wadudu kwa sababu wanaweza kuharibu mali, kusababisha hatari kwa afya au kuwa na usumbufu tu. Viuadudu vinatajwa kuwa sababu muhimu ya kuongezeka kwa tija ya kilimo ya karne ya 20. [2]

Lakini matumizi ya viuadudu huwa na hatari ya kuvuruga ekolojia na hivyo kuathiri mazingira ya wanyama na mimea. Viuadudu vingi ni sumu pia kwa wanyama wasio wadudu na pia kwa binadamu. Kuna viuadudu vinavyokolea katika mfuatano wa ulishano (food chain).

Aina za viuadudu

Viuadudu hugawiwa katika vikundi viwili vikubwa:

  • madawa ya kimfumo, ambayo yanasambaa katika mazigira na kuwa na athira ya muda mrefu;
  • madawa ya mgusano, ambayo yanaathiri wadudu kwa kipindi kifupi.

Viuadudu asilia

Mimea mbalimbali hutengeneza viuadudu asilia ambavyo ni kinga ya mimea hiyo dhidi ya kushambuliwa na wadudu. Utomvu wa misonobari ni namna ya kiuadudu asilia.[3] Mara nyingi harufu ni kinga kinachozuia mdudu kula mmea-

Aina kadhaa za mimea hutumiwa kibiashara kwa kutengeneza viuadudu:

[4]

Viuadudu vya kikemikali

Tangu siku za kale kemikali chache ziliwahi kutumiwa kuzuia au kuua wadudu waharibifu, hasa katika kilimo. Kati ya dawa hizo kulikuwa na sulfuri na asenia. Tangu mwisho wa karne ya 19 kemia imewezesha kutengeneza dawa mbalimbali za kuua au kudhibiti wadudu. Dawa hizo zimeleta mafanikio makubwa na kuongeza mavuno ya mazao duniani, na hivyo kusaidia kulisha idadi kubwa ya watu.

Lakini mara nyingi ilionekana baadaye kwamba maendeleo hayo yalikuja sambamba na hasara zilizotambuliwa baadaye.

Viuadudu vya kibiolojia

Kwa sababu viuadudu vya kemikali vina athari mbaya kwa mazingira mara nyingi, siku hizi viuadudu vya kibiolojia hutumika. Viuadudu hivi vina viambato asilia, k.m. vidubini au misindiko ya mimea. Kwa kawaida vinategenezwa kwa kukuza na kukusanya vidubini vinavyotokea uasiliani, labda pamoja na vifundiro vya metaboli vyao, k.m. bakteria, virusi, kuvu na protozoa. Nematodi hushirikishwa katika orodha hiyo ijapokuwa si vidubini kwa kweli. Dawa hizo zinachukuliwa mara nyingi kama visehemu shiriki vya miradi ya mchanganyiko wa udhibiti wa viharibifu (Kiing.: integrated pest management) na zinatumika zaidi na zaidi badala ya dawa za kikemikali.

Matatizo kwa mazingira

Athari kwa spishi zisizolengwa

Dawa nyingi za kikemikali huua hata spishi zisizolengwa. Kwa mfano, ndege wakila nafaka zilizonyunyiziwa kiuadudu wanaweza kupokea kiasi cha dawa kinachowaua.[5] Dawa za kunyunyizia huweza kupulizwa na upepo mbali na mashamba yaliyolengwa hadi eneo ambalo limetengwa kwa wanyamapori, hasa yakinyunyiziwa kwa eropleni.

DDT

DDT ilibuniwa katika miaka hadi 1940 kama dawa mbadala kwa sumu zilizowahi kutumiwa kama misombo ya risasi na ya asenia, ambayo yalikuwa katika matumizi ya kawaida.[6]. DDT ilionekana kuleta mafanikio makubwa ikatumika kwa wingi dhidi ya mbu wanaosambaza malaria au homa ya denge na baadaye ilipatikana pia kwa wakulima kote duniani na kwa matumizi ya nyumbani. Lakini ilionekana kwamba iliua pia wadudu walio muhimu kwa binadamu kama nyuki na hivyo kuhatarisha uzalishaji wa matunda; DDT ilikolea katika mfuatano wa ulishano kwa kusanyika kwenye tishu za mafuta za viumbe na kusababisha kudhoofika kwa maganda ya mayai ya ndege; spishi mbalimbali za ndege zilianza kupotea. Ilionekana pia kuleta hatari ya kansa kwa binadamu.[7]Matokeo hayo yalileta mapatano ya kimataifa ya Stockholm yanayokataza matumizi yake tangu mwaka 2004.

Usambazaji kupitia maji

Dawa ya kiuadudu, hasa ikiwa hutumika kwa kiasi kikubwa mno katika eneo fulani, husambazwa kwa mtiririko wa maji. Wakati theluji inapoyeyuka na mvua inanyesha na kupita ardhini, maji huchukua dawa za kuulia wadudu na kuzipeleka hadi mito, maziwa na mikusanyiko ya maji chini ya ardhi inayolisha tena chemchemi. [8] Kwa njia hiyo ubora wa vyanzo vya maji huathiriwa pamoja na ekolojia ya maeneo makubwa pamoja na afya ya wanadamu.

Kupungua kwa wachavushaji

Viuadudu vinaweza kuua nyuki na wachavushaji wengine, yaani wadudu wanaochavusha maua yaliyo msingi wa matunda. Katika nchi mbalimbali idadi ya nyuki imeshapungua mno[9]. Kupotea kwa wadudu wachavushaji kunaleta upungufu wa mavuno ya mazao. Hata viwango vidogo vya viuadudu huathiri tabia ya kuzindua nyuki. [10] Walakini, utafiti juu ya sababu za kupotea kwa nyuki huko Marekani haukuleta bado matokeo ya uhakika hadi mwaka 2007. [11]

Kupungua kwa ndege

Licha ya athari za matumizi ya viuadudu ya moja kwa moja, ndege waladudu huanza kupotea kwa sababu ya kupungua kwa mawindo yao. Kunyunyizia ngano na mahindi hususan huko Ulaya inaaminika kusababisha kushuka kwa asilimia 80 ya wadudu wanaoruka. Badiliko hilo limepunguza idadi ya ndege kwa karibu theluthi moja hadi mbili. [12]

Njia mbadala

Badala ya kutumia dawa za kikemia kwa kuzuia uharibifu wa mazao yanayosababishwa na wadudu, kuna njia mbadala zinazopatikana sasa ambazo zinaweza kuwalinda wakulima dhidi ya hasara kubwa. [13] Baadhi yao ni:

  1. Kuzalisha mazao sugu zaidi, au angalau mazao yasiyoshambuliwa haraka na wadudu. [14]
  2. Kudhibiti wadudu kwa njia ya kibiolojia, kwa kutumia waladudu, vimelea au pathojeni kupunguza idadi ya wadudu [15]
  3. Kutumia mbinu za kikemia ambazo hazina sumu, kama vile kemikali zinazochanganya wadudu wasiweze kutambua wenzi wao; hivyo wengi wanashindwa kuzaliana. [16]

Marejeo

Kujisomea zaidi

  • McWilliams, James E., " 'Horizon Kufunguliwa Up Sana Sana': Leland O. Howard na Transition kwa Chemical Insecticides nchini Marekani, 1894-1927," Historia Kilimo, 82 (Fall 2008), 468-95.

Viungo vya nje

Simple English Wiktionary
Wikamusi ya Kiswahili ina maelezo na tafsiri ya maana ya neno: