Homo

Homo
Fuvu la kichwa katika Mkusanyo wa Palantolojia wa Makumbusho ya Kitaifa ya Ethiopia
Fuvu la kichwa katika Mkusanyo wa Palantolojia wa Makumbusho ya Kitaifa ya Ethiopia
Uainishaji wa kisayansi
Domeni:Eukaryota
Himaya:Animalia (Wanyama)
Faila:Chordata (Wanyama wenye ugwe wa neva mgongoni)
Ngeli:Mamalia (Wanyama wenye viwele wanaonyonyesha wadogo wao)
Oda:Primates (Wanyama wanaofanana kiasi na binadamu)
Familia ya juu:Hominoidea (Wanyama kama binadamu)
Familia:Hominidae (Walio na mnasaba na binadamu)
Nusufamilia:Homininae (Wanaofanana sana na binadamu)
Kabila:Hominini
Jenasi:Homo
Linnaeus, 1758
Ngazi za chini

Spishi 12:

  • H. antecessor Bermudez de Castro, Arsuaga, Carbonell, Rosas, Martinez & Mosquera, 1997
  • †H. erectus Dubois, 1894
  • †H. ergaster Groves & Mazak, 1975
  • †H. floresiensis Brown, Sutikna, Morwood, Soejono, Jatmiko, Saptomo & Due, 2004
  • †H. habilis Leakey, Tobias & Napier, 1964
  • †H. heidelbergensis Schoetensack, 1908
  • †H. longi Ji et al., 2021
  • †H. luzonensis Détroit et al., 2019
  • †H. naledi Berger et al., 2015
  • H. neanderthalensis King, 1864
  • †H. rudolfensis Alekseev, 1986
  • H. sapiens Linnaeus, 1758
Uenezi wa binadamu nje ya Afrika, kufuatana na ADN ya dutuvuo (mitokondria). Duara za rangi mbalimbali zinamaanisha maelfu ya miaka kabla ya leo.
Uenezi wa binadamu nje ya Afrika, kufuatana na ADN ya dutuvuo (mitokondria). Duara za rangi mbalimbali zinamaanisha maelfu ya miaka kabla ya leo.

Homo ni jenasi ambayo katika uainishaji wa kisayansi inajumlisha binadamu na spishi zilizokwishakoma zilizofanana naye sana kibiolojia. Wanasayansi wamependekeza zaidi ya spishi 12 za jenasi Homo.

Jina Homo ni la Kilatini, likiwa na maana ya "mtu", na kwa asili linahusiana na neno humus, "ardhi".[1]

Historia ya awali

Uenezi wa jenasi Homo kwa wakati na mahali.
Homo katika miaka 600,000 ya mwisho (kutoka chini kwenda juu). [2] Homo heidelbergensis anaonyeshwa akigawanyika kati ya Waneanderthal, Wadenisova na H. sapiens. Baada ya H. sapiens kuenea kuanzia miaka 200,000 iliyopita, Waneanderthal na Wadenisova na wengineo wasiojulikana bado wanaonyeshwa kuungana na kumezwa na H. sapiens. Pia inaonyeshwa michanganyiko mingine iliyoweza ikawatokea Waafrika wa kisasa.

Jenasi hiyo imekadiriwa kuanza kuwepo miaka milioni 2.1 - 2.8 iliyopita[3][4] kutokana na spishi mojawapo ya nusukabila Australopithecina (siku hizi linatumika pia jina Hominina) iliyokuwepo kuanzia miaka milioni 5.6 hadi 1.2 iliyopita.

Spishi ya kwanza ya jenasi hiyo inawezekana ilikuwa ile ya Homo habilis, yaani mtu mwenye uwezo wa kutengeneza vifaa. Mabaki yake yalipatikana huko Oltupai (Tanzania). Huyo anafikiriwa kutokana na Australopithecus garhi ambaye kabla yake alikuwa ameanza kutengeneza vifaa kwa mawe.

Hata hivyo mnamo Mei 2010 huko Afrika Kusini yalipatikana mabaki ya Homo gautengensis, spishi inayofikiriwa na wengine kuwa ya kale kuliko Homo habilis[5], lakini wengine wanaijumlisha katika jina Homo habilis. Tena wataalamu wengine wanaona spishi hizo mbili hazistahili kuitwa Homo, ila Australopithecus.

Kutokana na Homo habilis (au Australopithecus habilis) alipatikana miaka milioni 2 iliyopita Homo erectus aliyekuwa wa kwanza kusimama daima juu ya miguu yake miwili, kuwinda na kumudu moto, na ambaye alienea kote Asia na Ulaya (aliyebaki Afrika anaitwa pia Homo ergaster) kabla ya kugawanyika katika nususpishi au spishi mpya mbalimbali kama Homo georgicus, Homo antecessor, Homo heidelbergensis, wa kwanza kujenga makazi ya kudumu na kuzika wafu, n.k. Kwa jumla Homo erectus alidumu zaidi ya miaka milioni moja. Wengi wanaona spishi nyingi zilizopendekezwa kuwa nususpishi tu za Homo erectus.

Miaka 800,000–200,000 iliyopita, wakati wa mabadiliko makubwa ya hali ya hewa, ubongo wa jenasi hiyo ulikua sana na kupata uwezo wa kufanya mambo mengi mapya katika mahusiano na katika kukabili mazingira ambayo yalizidi kubadilika na kudai maitikio tofauti ili kudumisha uhai wa jenasi yenyewe.

Kufikia miaka 100,000 au 50,000 hivi iliyopita, spishi zote za jenasi Homo zilikuwa zimekoma, isipokuwa Homo sapiens aliyekuwa ametokana na Homo heidelbergensis miaka 300,000 hivi iliyopita.

Baadhi ya wataalamu wanahesabu Homo neanderthalensis na mtu wa Denisova kama nususpishi za Homo sapiens zilizoweza kuzaliana na watu wa kisasa waliotokea Afrika.[6][7][8]

Picha

Tanbihi

Marejeo

Viungo vya nje

Wikimedia Commons ina media kuhusu: